SUA fanyeni tafiti juu ya mbegu za miti rafiki wa maji - Dkt. Selemani Jafo

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Mhe. Dkt.  Selemani Jafo amewaomba wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA kuzidi kufanya tafiti juu ya mbegu za miti rafiki wa maji ili zikazalishe miche itakayosaidia katika utunzaji wa vyanzo vya maji vilivyoathirika.

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Dkt.  Selemani Jafo (katikati) akiwa na tuzo aliyokabidhiwa katika Majalisi ya SUA

Dkt. Jafo ameyazungumza hayo Novemba 24, 2022 mjini Morogoro wakati wa Majalisi ya SUA yaliyofanyika katika Kampusi Kuu ya Edward Moringe ambapo amesema wataalamu waangalie miti ya asili yenye sifa ya kuhifadhi maji ikatumike katika kurejesha uhalisia wa mito katika baadhi ya maeneo.

“Mbinu ambayo nimefikiria ni kuzifanya shule zetu za msingi na sekondari ziwe vituo vya kuzalishia miche ili iwe rahisi kwa maeneo mengi kupata miche hiyo lakini changamoto ni upatikanaji wa mbegu hivyo tafiti ziendelee kufanyika ili mradi tuweze kupata mbegu za kutosha na kwa gharama nafuu zitakazosaidia kuikoa nchi”, alisema Dkt. Jafo.

Aidha Dkt. Jafo ameipongeza SUA  kwa tafiti zake ambazo zinafanya kilimo kuwa na tija na kutoa mchango mkubwa katika Sekta ya Kilimo nchini na amewataka wahitimu wanaohitimu masomo yao wanapopewa nafasi ya kazi basi kwenda kufanya kazi kwa juhudi na maarifa ili kuzijengea heshima Taasisi zilizowajengea maarifa.

“Kwa kuwa mnalipwa mshahara basi nendeni mkafanye kazi na kuacha uvivu kafanye kazi asipatikane wa kuvaa viatu vyako utakapoondoka, mfanye kazi kama ibada kwamba usipotimiza wajibu wako mungu atakuhukumu kwa kuwa kuna watu wanahitaji msaada mkubwa sana hivyo wewe msomi umepata fursa basi wasaidie”, alisema Dkt. Jafo.

 

 

 

Share this page