Mafundi sanifu wa maabara wajengewa uwezo SUA

Mafundi sanifu wa maabara za kupima Ubora wa Bidhaa zitokanazo na Mimea dawa kutoka Taasisi mbalimbali nchini wametakiwa kushirikiana katika kazi zao ili kuhakikisha bidhaa zinazozalishwa nchini zinafikia soko la kimataifa na kuchangia katika pato la watengenezaji na taifa.

SUA

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Shahada za Juu, Utafiti, Uhaulishaji wa teknolojia na Ushauri wa kitaalamu Prof. Esron Karimuribo siku ya Jumanne, 28 Juni 2022, wakati akifunga mafunzo ya siku nne yaliyohusu namna ya kutumia vifaa vya kisasa vya upimaji ubora. 

“Sisi sote tunajenga Taifa moja, hatushindani sisi kwa sisi hivyo ni wajibu wetu kushirikiana katika kazi zetu ili kusaidia kufanikisha jukumu tulilopewa la kusimamia ubora na hasa pale inapotokea changamoto kwa mmoja wenu muwe tayari kusaidiana ili kazi zifanyike kwa ufanisi” alifafanua Prof. Karimuribo.

Prof. Esron Karimuribo

Naye kiongozi wa mafunzo hayo kutoka Chuo Kikuu cha Copenhagen nchini Denmark Prof. Bjarne Styrishave amesema mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa GRILI na Shirika la Misaada la maendelo la Denmark DANIDA ambayo kwa pamoja yanasisitiza umuhimu wa uchunguzi wa viwango vya kemikali kwenye mimea dawa ili kulinda afya ya watumiaji.

“Ili malengo hayo yatimie lazima Tanzania iwe na wataalamu wengi na wenye uwezo wa kutumia vifaa vya kisasa vya uchunguzi maana teknolojia zinakua kila siku lakini pia mafundi hao wawe na uwezo wa kuvifanyia matengenezo madogomadogo pale vinapopata hitilafu badala ya kuvitupa au kuhitaji kupelekwa nje ya nchi kwa matengenezo hivyo mafunzo haya sasa yamewapa uwezo huo na kupitia ushirikiano wataweza kufanya kazi zao vizuri” alibainisha Prof. Bjarne.

Amesema kwenye mafunzo hayo ameona mchanganyiko wa wataalamu kutoka Taasisi mbalimbali nchini inagwa inawezekana wengine hawafanyi kazi za kupima ubora wa bidhaa za mimea dawa lakini jambo kubwa na la msingi wanafanya kazi za kufanya uchunguzi wa ubora wa vitu mbalimbali na kifaa cha kisasa zaidi duniani ni LC/MS ambacho kimefundishwa na kipo SUA.

Amesema kupitia DANIDA wameweza kukamilisha maabara nzuri na kuweka vifaa vya kisasa kama vile LC/MS/MS vya upimaji ubora na viambata katika mimea dawa lakini mafunzo haya ni sehemu ya kuhakikisha uwezo na uchunguzi wa ubora wa bidhaa mbalimbali nchini unakuwa endelevu maana mradi ni wa miaka mitano lakini shughuli hizo zinatakiwa kuendelea hata pale mradi utakapomalizika.

Awali akieleza malengo ya Mafunzo katika mradi huo, Mkuu wa Mradi wa GRILI Dkt. Faith Mabiki amesema mafunzo hayo yanalenga katika lengo la msingi la kwanza la mradi huo la kuhakikisha wanajengea uwezo wataalamu kwenye matumizi ya vifaa na uwezo wa kupima ubora na kemikali za mimea dawa.

“Mradi umesaidia kusomesha wanafunzi sita wa Shahada ya Uzamivu na wanafunzi wawili wa shada za Uzamili na bado tunaendelea kuona ni namna zipi tunaweza kuzitumia kuhakikisha kazi hii inaendelea baada ya mradi kuisha na mkakati wetu wa kwanza ni ushirikiano ndio maana tumewaita Mafundi sanifu hawa kutoka taasisi mbalimbali nchini wanaofanya kazi hizi wafahamiane na kujenga ushirikiano” aifafanua Dkt. Mabiki.

Mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo kutoka Chuo cha Ufundi Arusha Bwana Meshack Timoth na Mkuu wa Maabara ya upiamaji Ubora wa  Udongo, Maji na mimea ameshukuru kupata nafasi ya kushiriki mafunzo hayo ambayo yamefanyika kwa vitendo zaidi katika kutumia kifaa hicho cha kisasa kilichopo SUA.

“Pamoja na kujifunza lakini mafunzo yametupatia nafasi ya kufahamiana na kushirikiana miongoni mwetu kutoka taasisi mbalimbali na hii itatusaidia kutatua changamoto mbalimbali zinapotokea miongoni mwetu” Alieleza Fundi sanifu huyo wa maabara Bwana Timoth.

Naye Mshiriki kutoka Mamlaka ya maabara ya Mkemia mkuu wa Serikali Bwana Edward Dilunga amesema mafunzo hayo yamewasaidia kuwaongezea ujuzi katika utekelezaji wa majukumu yao hasa ikizingatiwa kuwa sayansi inakua na teknolojia mpya zinazalishwa kila siku hivyo mafunzo hayo yataongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Kwangu mimi binafsi kama Mkemia imeniongezea ujuzi zaidi ya ule niliokuwa nao katika uchakataji wa Sampuli kwa kutumia kifaa hiki cha kisasa cha LC/MS HP/LC ambavyo vyote hivi ni vifaa ambavyo kwenye Ofisi ya Mkemia mkuu wa Serikali vipo lakini ni faida kwa taasisi yangu maana elimu niliyoipata itasaidia kuboresha utendaji wangu na kuleta matokeo chanya katika ofisi yangu,” alieleza Bwana Dilunga.

Kwa upande wake Afisa mthibiti Ubora kutoka Shirika la Viwango Tanzania (TBS) Bi. Tatu Yusufu amesema mafunzo yamemsaidia kuongeza uwezo kwenye kutumia HPLC mashine ambayo wameanza kuitumia kwa sasa kwenye maabara yao na GC ambayo anaitumia hivyo mafunzo yamekuwa na msingi mno katika kazi zao.

“Sisi TBS hatutumii HPLC /MS na TC kwahiyo hapa nimeongezewa ujuzi mpya wa kuchanganya mashine hizo zote kwa pamoja kwenye matumizi na hivyo nimeona kuwa HPLC/MS kwa pampja inafanya vizuri zaidi kuliko ukizitengenisha”Alifafanua Bi.Tatu.

Tukio hilo lilifanyika siku ya Jumanne ya tarehe 28 Juni 2022 kwenye ukumbi wa mikutano uliopo kampasi ya Solomon Mahlangu, Mazimbu mkoani Morogoro.

Imeandikwa na Calvin Gwabara - SUAMEDIA
 

Share this page